IQNA

Iran haijapokea mwaliko wa Saudia kuhusu vikao vya Hija

10:04 - January 07, 2017
Habari ID: 3470782
IQNA: Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amekanusha madai kuwa Iran imepokea mwaliko wa Saudia wa kushiriki katika vikao kuhusu Hija mwaka huu. Bahram Qasemi amesema, kama ilivyotangazwa huko nyuma, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran hadi hivi sasa haijapokea barua yoyote kutoka kwa Saudi Arabia.
Iran haijapokea mwaliko wa Saudia kuhusu vikao vya Hija
Amesema: Kwa mara nyingine tunapenda kusisitiza kwamba, ni jambo lililo wazi kuwa, kama mwaliko huo utatolewa na mazingira yakawa yanaruhusu, basi suala la kutumwa mahujaji litashughulikiwa na taasisi husika na vyombo hivyo ndivyo vitakavyochukua maamuzi.
Siku chache zilizopita kulikuwa na taarifa kuwa, Wizara ya Hija ya Saudi Arabia imezitumia barua nchi 80 duniani ikiwemo Iran kuzialika kushiriki katika mjadala wa kufanikisha ibada ya Hija mwaka huu.
Gazeti la al Hayat linalochapishwa London limeandika kuwa Waziri wa Hija wa Saudia Mohammed Bentin imeanza mazungumzo na zaidi ya nchi 80, ikiwemo Iran, kuhusu mipango ya Ibada ya Hija mwaka 2017.Gazeti hilo limeandika kuwa, 'ujumbe wa Iran umealikwa Saudia kwa ajili ya mazungumzo.'Maafisa wa Iran hadi sasa hawajatoa tamko lolote kuhusu ripoti hiyo.
Hata hivyo Taasisi ya Hija na Ziara ya Iran imesema, haijapokea barua yoyote kutoka kwa Wizara ya Hija ya Saudi Arabia.
Itakumbukwa kuwa Septemba 2015, kulitokea msongamano mkubwa wa Mahujaji wakati wa Ibada ya Hija huko Mina karibu na Makka. Saudia ilidai kuwa wau 770 walipoteza maisha katika msongamano huo. Hatahivyo Iran ilitangaza kuwa Mahujaji 4,700, wakiwemo Wairani 465 walipoteza maisha katika tukio hilo. Kabla ya hapo pia mahujaji wengine 100 walipoteza maisha, wakiwem Wairani 11 wakati winchi ilipoanguka katika Masjidul Haram.
Kufuatia matukio hayo, Iran ilitaka usalama wa Mahujaji udhaminiwe lakini Saudia ilikataa kushirkiana katika suala hilo na hatimaye wakuu wa Saudia wakawazuia mahujaji Wairani kutekeleza ibada ya Hija mwaka 2016.
Watawala wa Saudia wanaluamiwa kwa usimamizi mbovu wa Ibada ya Hija jambo ambalo limepelekea idadi kubwa ya mahujaji kupoteza maisha kila mwaka.
Waislamu duniani wamekuwa wakitaka utawala wa Saudia uzishirikishe nchi zenye idadi kubwa ya mahujaji katika usimamizi wa Ibada ya Hija ambayo ni nguzu muhimu ya Uislamu.
Mkuu wa Shirika la Hija la Iran mwezi Septemba alisema ni jambo lisilokubalika kwa Saudia kuwauzia Wairani kuhiji hasa kwa kuzingatia kuwa kuna Wairani ambao wako katika orodha ya kusubiri Kuhiji miaka 15 hadi 20 ijayo. Ameongeza kuwa, Saudia inaamini kuwa miji mitakatifu ya Makka na Madina ni milki yake katika hali ambayo maeneo hayo matakatifu ni milki ya Waislamu wote.
captcha