Kwa mujibu wa mwandishi wa IQNA, mitindo ya vazi la staha la Hijabu ni kati ya mitindo yanye kuenea kwa kasi zaidi barani Ulaya na hasa Uingereza na kuna soko kubwa la wanunuzi.
Washonaji wa mitindo ya Hijabu wanazingatia Imani ya Kiislamu na huwalenga wanawake Waislamu. Aidha wanawake wa dini na tamaduni nyinginezo ambao wanataka kujistiri nao pia wanavutiwa na mitindo ya Hijabu.
Wabunifu wa nguo na mitindo (fashion designer) wapatao 40 walionyesha mavazi yao katika maonyesho hayo ya wiki hii.
Kati wa wabunifu wa nguo na mitindo walioshiriki ni Bi.Bushra Sheikh wa London ambaye alama ya nguo zake ni iiLa na ilianzishwa miaka sita iliyopita ambapo hivi sasa anaunza nguo zake kote duniani.
Hivi sasa anafanya mazungumzo na maduka makubwa mjini London ili yaweze kuuza nguo zake kwani anaamini kuwa kuna soko kubwa la mitindio ya Hijabu aliyobuni.
Mratibu wa maonyesho hayo, Bi.Romanna Bint-Abubaker anasema soko la Waislamu ndilo linalostawi kwa kasi zaidi duniani huku akitabiri kuwa ifikapo mwaka 2030, katika kila watu watatu duniani moja atakuwa ni Mwislamu. Kwa msingi huo, Bint-Abubaker ambaye nia mwanzilishi wa tovuti ya Haute Elan ya mitindo ya Hijabu, anasema kuna haja ya kubuni mitindo ya kutumiwa na wanawake Waislamu.
Imearifiwa kuwa duka la Debenhams litakuwa duka la kwanza kubwa kuuza mavazi ya Hijabu ya wanawake Waislamu kote Uingereza. Aidha maduka kadhaa ya nguo katika miji ya London, Manchester na Leicester yataanza kuuza mavazi ya Hijabu nchini Uingereza.