Kwa mujibu wa mwandishi wa IQNA, msafara huo umefika Tanzania kwa ushirikiano wa Mwambata wa Utamaduni wa Iran mjini Dar es Salaam kwa lengo la kushiriki katika sherehe za Wiladat ya Imam Ridha AS katika nchi hiyo ya Afrika Mashariki.
Jumanne Agosti Mosi ulifika katika ukumbi wa Ofisi ya Mwambata wa Utamaduni wa Iran mjini Dar es Salaam ambapo kulikuwa na mjumuiko mkubwa wa wafuasi na muhibina wa Ahul Bayt AS. Katika sherehe hiyo kulikuwa na hotuba pamoja na qaswida kwa munasaba wa Wiladat ya Imam Ridha AS.
Msafara huo pia ulifika katika Msikiti wa Al Ghadir eneo la Kigogo Dar es Salaam ambapo baada ya Sala za Magharibi na Ishaa, waliokuwa katika msafara huo walisoma Qur’ani Tukufu na Dua Tawassul. Akihutubu katika hafla hiyo, Bw. Ali Bagheri, Mwambata wa Utamaduni wa Iran nchini Tanzania aliukaribisha msafara huo kutoka Haram ya Imam Ridha AS na kusema: "Imam Ridha AS ni kutoka katika kizazi cha Mtume Muhammad SAW na ni imamu anayeheshimiwa na Waislamu wote wa madhehebu za Shia na Sunni.” Aidha kikao hicho kilihutubiwa pia na Hujjatul Islam Khusropanah ambaye alibainisha nafasi na hadhi ya Uimamu katika Uislamu. Katika hafla hiyo pia kulizinduliwa bendera ya Haram Takatifu ya Imam Ridha AS ambapo hadhirina walipata fursa ya kutabaruku. Msafara huo pia ulipata fursa ya kumtembelea Balozi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran nchini Tanzania Mheshimiwa Musa Farhang.
Itakumbukwa kuwa, 11 Dhil-Qaadah mwaka 148
Hijiria, alizaliwa mjini Madina, Imamu Ali Bin Musa al-Ridha (as), mmoja wa
Ahlu Bayti watukufu wa Mtume Muhammad SAW na imamu wa nane wa Waislamu. Imamu
Ridha AS alianza kuongoza umma wa Kiislamu mwaka 183 baada ya kufariki dunia
baba yake mtukufu, yaani Imamu Musa al-Kaadhim AS. Katika uhai wake alifahamika
kama shakhsia wa pekee katika ulimwengu wa Kiislamu kutokana na elimu yake ya
hali ya juu na uchaji-Mungu.