IQNA

Hassan Rouhani aapishwa kuwa rais waJamhuri ya Kiislamu ya Iran kwa muhula wa pili

22:30 - August 05, 2017
Habari ID: 3471106
TEHRAN (IQNA)-Hassan Rouhani jioni ya leo amekula kiapo cha kuwa rais wa 7 wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwa kipindi kingine cha miaka minne kwa kuahidi mbele ya Qur'ani tukufu kwamba atalinda Uislamu, Mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu na Katiba ya nchi.
Rais Hassan Rouhani amekula kiapo hicho mbele ya kitabu kitakatifu cha Qur'ani katika sherehe iliyofanyika katika ukumbi wa Bunge la Jamhuri ya Kiislamu na kuhudhuriwa na Mkuu wa Idara ya Mahakama, Ayatullah Sadiq Amoli Larijani, wawakilishi wa Bunge, wanachama wa Baraza la Kulinda Katiba na wageni waalikwa kutoka nje ya nchi.

"Nitalinda dini rasmi ya nchi hii, Utawala wa Jamhuri ya Kiislamu na Katiba ya Iran, na nitatumia nguvu na mamlaka yangu katika kutekeleza majukumu niliyopewa na kujisabilia kwa ajili ya kuhudumia wananchi, kustawisha nchi, kueneza dini na maadili, kuunga mkono haki na uadilifu, na kujiepusha na udikteta. Nitatetea uhuru na heshima za watu na haki za taifa zilizoainishwa na Katiba", amesema Rais Rouhani wakati anaapisha bungeni.

Baada ya kuapishwa rasmi, Rais Rouhani alitia saini hati ya kiapo mbele ya Mkuu wa Idara ya Mahakama hapa nchini na wajumbe wa Baraza la Kulinda Katiba. Hassan Rouhani aapishwa kuwa rais Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwa muhula wa pili

Sherehe za kuapishwa Rais Rouhani zimehudhuriwa na marais, maspika wa mabunge, mawaziri wakuu, mawaziri wa nchi za nje, Mkuu wa Sera za Kigeni za Umoja wa Uyala na wawakilishi wa zaidi ya nchi mia moja. 

Siku ya Alhamisi Sherehe ya kuidhinisha kura za wananchi kwa Rais wa Jamhuri ya Kiislamu zilifanyika asubuhi katika Husseiniya ya Imamu Khomeini MH hapa Tehran kwa Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu kumpasisha Hassan Rouhani kuwa Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.

Kwa mujibu wa kifungu cha 110 cha Katiba ya Iran, miongoni mwa majukumu na mamlaka ya Kiongozi Muadhamu ni kusaini na kupasisha dikrii ya Rais wa nchi baada ya kuchaguliwa na wananchi. Kipindi cha urais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ni miaka minne na Rais huanza kutumikia wadhifa wake baada ya tarehe ya kuidhinishwa hati za utambulisho wake na Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu.

Hassan Rouhani kwa mara nyingine tena alichaguliwa kuwa Rais wa Iran katika duru ya 12 ya uchaguzi wa Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran uliofanyika Mei 19 mwaka huu kwa kupata kura zaidi ya milioni 23.

3626992

captcha