Katika ujumbe wake aliomtumia Hujjatul Islam Sayyid Murtada Murtada al-Amili, ndugu yake Allahmah Sayyid Ja'far al-Amili, Ayatullah Sistani amebainisha masikitiko yake kufuatia kuaga dunia mwanazuoni huyo mkubwa wa Kiislamu.
Sehemu ya ujumbe huo imesema: "Hujjatul Islam wa Muslimin Sayyid Jaʿfar Murtaḍa al-Amili alipitisha umri wake uliojaa baraka katika kuwahudumia Ahul Bayt AS na kuwatetea sambamba na kuandika vitabu vya maarifa yao."
Ayatullah Sistani amemuomba Mwenyezi Mungu SWT amjaalie Marhum Allamah Jaʿfar Murtaḍa al-Amili awe na mababu zake watoharifu na awape subira na utulivu jamaa na marafiki zake.
Inafaa kuashiria hapa kuwa, Allamah Al-Sayyid Jaʿfar Murtaḍa al-Amili alikuwa miongoni mwa wanazuoni wakubwa katika vyuo vya kidini nchini Lebanon na mjini Qum, Iran na alibobea katika historia ya Uislamu na madhehebu ya Shia. Allamah Al-Sayyid Jaʿfar Murtaḍa al-Amili aliaga dunia 26 Oktoba wakati akipata matibabu hospitalini mjini Beirut. Alikuwa na umri wa miaka 74 wakati alipoaga dunia.
Kati ya vitabu vingi alivyoandika kuhusu historia ya Uislamu na itikadi za Kishia tunaweza kutaja Al-Sahih min sirat al-Nabi al-A'zam, Ma'sat al-Zahra' (a), Al-Sahih min sirat al-Imam 'Ali (a), Al-Ziwaj al-muwaqqat fi l-Islam "al-Mut'a" (dirasat wa tahlil), Al-Wilaya al-tashri'iyya, Al-Shahadat al-thalitha fi l-adhan wa l-iqama (shubahat wa rudud), Marasim 'Ashura (shubahat wa rudud) , na Mizan al-haqq.