IQNA

Maelfu nchini Yemen washiriki katika Maulid ya Mtume Muhammad SAW

11:49 - November 10, 2019
Habari ID: 3472208
TEHRAN (IQNA) – Makumi ya maelfu ya watu wa Yemen wameshiriki katika sherehe za Maulid ya Mtume Muhammad SAW katika miji mbali mbali ya nchi hiyo ambayo ingali inakabiliwa na hujuma kijeshi ya utawala dhalimu wa Saudi Arabia.

Kwa mujibu wa taarifa, katika mji mkuu Sanaa, maelfu ya watu walimiminika katika Medani ya Al Sabeen, iliyo karibu na Msikiti wa Al Sha'ab kusherehekea kumbukumbu ya kuzaliwa  Mtume Muhammad SAW. Aidha sherehe hizo zimefanyika kwa munasaba wa kuanzi Wiki ya Umoja wa Kiislamu.

Ahlu Suna wal Jamaa wanategemea baadhi ya riwaya katika kuamini kwamba Mtume Mtukufu SAW alizaliwa tarehe 12 Rabiul Awwal nao Waislamu wa madhehebu ya Shia wana riwaya nyingine nyingi zinazowafanya waamini kuwa Mtume SAW alizaliwa tarehe 17 Rabiul Awwal. Kipindi cha kati ya tarehe hizo mbili kilitangazwa na Imam Khomeini MA, muasisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, kuwa Wiki ya Umoja wa Kiislamu ili kuleta umoja na mfungamano kati ya Waislamu bila kujali madhehebu zao.

Akizungumza katika sherehe hizo za Maulid ya Mtume SAW mjini Sanaa, Kiongozi wa wa Harakati ya Ansarullah ya Yemen ameuonya vikali muungano vamizi wa kijeshi unaoongozwa na Saudi Arabia dhidi ya nchi hiyo na kusisitiza kuwa, wavamizi hao wataendelea kuandamwa na vipigo na wajiandae kwa matokeo mabaya ya uvamizi wao.

Ameongeza kuwa, "Utawala wa Saudia usitishe uvamizi na mzingiro mara moja, vinginevyo madhara makubwa ya uvamizi huo yatakawakumba."

Amesema wavamizi hao wameshindwa kufikia malengo yao kutokana na kusimama kidete wananchi wa Yemen na kueleza bayana kuwa, vikosi vya Yemen vitaendelea kuimarisha zana zao za kijeshi na kutoa majibu makali iwapo Saudia na waitifaki wake wataendeleza uvamizi dhidi ya taifa la Yemen.

Abdul-Malik al-Houthi amefichua kuwa Saudia na Imarati zimeiba zaidi ya mapipa milioni 120 ya mafuta kusini mwa Yemen.

Kwengineko katika hotuba yake, Kiongozi wa Harakati ya Ansarullah ya Yemen ameashiria kuhusu maandamano yanayoendelea kushuhudiwa katika nchi za Lebanon na Iran na kubainisha kuwa, "Nayaasa mataifa ya eneo la Asia Magharibi yawe macho na yatatue mizozo iliyopo kwa umakini, ili yasitumbukie katika mtego wa njama za maadui."

Kadhalika amesema wananchi wa Yemen hawatachelewa kutoa jibu kali kwa utawala haramu wa Israel, iwapo Tel Aviv itakula njama yoyote ya kulishambulia taifa hilo la Kiarabu.

3469838

captcha