IQNA

Palestina

Mkutano wa Kimataifa wa Al-Quds kufanyika nchini Jordan

23:13 - September 24, 2022
Habari ID: 3475834
TEHRAN (IQNA) – Jordan itakuwa mwenyeji wa mkutano wa kimataifa kuhusu mji mtakatifu wa Al-Quds (Jerusalem) mwezi ujao.

Kikao hicho kimepangwa kufanyika tarehe 23-24 Oktoba, chini ya kaulimbiu ya “Al-Quds: Historia, Ubinadamu na Dini.”

Wizara ya utamaduni ya nchi hiyo ya Kiarabu itaandaa hafla hiyo kwa ushirikiano na Kituo cha Kimataifa cha Majadiliano ya Dini Mbalimbali chenye makao yake makuu mjini Doha na Umoja wa Kimataifa wa Wanazuoni wa Kiislamu.

Rasmi al-Falah, afisa wa kamati ya maandalizi, alisema zaidi ya wasomi 100, watafiti, wanafikra, watu wa kisiasa, maulama wa Kiislamu na Kikristo, na wawakilishi kutoka mashirika ya kimataifa na wanaharakati wa mashirika ya kiraia watashiriki katika mkutano huo.

Amesema makala 20 za kitaaluma zitawasilishwa na kujadiliwa katika mkutano huo, ikiwa ni pamoja na moja kuhusu uungaji mkono wa Jordan kwa al-Quds na jukumu lake katika kulinda maeneo matukufu ya Kiislamu na Kikristo katika mji huo.

Hadhi ya kihistoria ya al-Quds, demografia ya mji huo, utambulisho wake wa Kiarabu, umuhimu wake wa kidini, majukumu ya mashirika ya kimataifa, kieneo, kisiasa na haki za binadamu kuelekea mji huo, na nafasi ya vyombo vya habari katika kutoa ufahamu kuhusu maendeleo yake ni miongoni mwa mada zitakazojadiliwa katika hafla hiyo ya siku mbili, aliendelea kusema.

Jordan ndiye mlinzi wa maeneo matakatifu katika eneo la Msikiti wa Al-Aqsa huko al-Quds.  Mji wa Quds uliko msikitu huo wa Al Aqsa, ambao ni eneo la tatu kwa utukufu katika Uislamu, unakaliwa kwa mabavu na utawala dhalimu wa Israel kinyume cha sheria za kimataifa.

3480602

captcha