Rais Essebsi amechukua hatua hiyo kupitia hotuba aliyoitoa kufuatia shambulio hilo, ambapo sambamba na kulaani hujuma hiyo ya kigaidi, ametangaza hali ya kutotoka nje kuanzia saa tatu za usiku hadi saa 11 alfajiri. Akisisitiza kuwa, hivi sasa Tunisia iko katika vita dhidi ya ugaidi, amesema kuwa kufuatia hali hiyo serikali imejizatiti kulipatia jeshi la nchi hiyo kila aina ya zana zitakazotumika katika vita hivyo. Kwa mujibu wa duru za ikulu ya rais wa Tunisia, askari 20 wa gadi ya rais wameuawa katika shambulizi hilo la kujiripua lililolenga basi la askari hao. Kundi la kigaidi la ISIS au Daesh limedai kuhusika na hujuma hiyo.
Inaelezwa kuwa, mtu aliyekuwa amevalia mada za miripuko alikuwa ndani ya basi hilo kabla ya kujirupua na kusababisha maafa hayo hapo jana. Tunisia imekuwa ikikumbwa na vitendo vya kigaidi huku raia wake wengi wakiwa ndio wanaounda asilimia kubwa ya wanachama wa kundi la kigaidi na kitakfiri la ISIS huko nchini Iraq na Syria.