IQNA

Mufti wa Misri: Daesh (ISIL) wanaelewa vibaya Uislamu

20:52 - February 13, 2015
Habari ID: 2846216
Sheikh Shawki Ibrahim Abdulkarim Allam Mufti Mkuu wa Misri amesema kuwa, kundi la kigaidi la Daesh (ISIL) ni kundi hatari mno na kusisitiza kwamba kundi hilo la kitakfiri na kigaidi halifungamani kabisa na matukufu ya dini ya Kiislamu na lina fikra na uelewa potofu kuhusiana na dini ya Kiislamu.

Akizungumza na gazeti la al Ahram linalochapishwa nchini Misri, Mufti Mkuu wa nchi hiyo amesisitiza kwamba dini ya Kiislamu imeweka misingi na sheria za kuhifadhiwa haki za mateka na kwamba Mtume Mtukufu (saw) daima alikuwa akiwausia Masahaba zake kuamiliana vyema na mateka. Mufti Mkuu wa Misri ameongeza kuwa wanamgambo wa kitakfiri na kigaidi wa Daesh wamekuwa wakiwauwa Waislamu kwa kuwakata vichwa na kuwachoma moto mateka wanaowashikilia, jambo ambalo ni kinyume na mafundisho ya Kiislamu. Sheikh Shawki Ibrahim Allam ameongeza kuwa, Mtume Mtukufu (saw) amesema kuwa, Mwenyezi Mungu ameharamisha kumwagwa damu ya mtu aliyetoa shahada ya kumuamini Mwenyezi Mungu mmoja na Muhammad (saw) ni Mtume wake, lakini magaidi wa Daesh wamekuwa wakiendeleza vitendo vya kikatili vya kuuawa, kubaka na kunajisi Waislamu na wasio Waislamu katika nchi za Syria na Iraq..../MH

2844145

Kishikizo: misri mufti daesh shawki
captcha