Akizungumza Jumatatu kupitia televisheni ya Al Masirah, Sayyid Abdul Malik Badurddin al Houthi, kiongozi wa Harakati ya Ansarullah nchini Yemen amesisitiza kuwa, eneo la Asia Magharibi (Mashariki ya Kati) limefikia kipindi ambacho baadhi ya nchi zinashirikiana na adui Mzayuni anayehujumu matukufu ya Kiislamu na ziko tayari kufanya kila njama dhidi ya Waislamu.
Abdul Malik al Houthi amesema kuwa, uhusiano wa siri wa serikali vibaraka katika eneo la magharibi mwa Asia na utawala wa Kizayuni wa Israel umetoka katika hali ya usiri na kudhihirika waziwazi na zinashiriki katika njama za Marekani na Israel kwa madai kwamba zinataka amani na usalama.
Al Houthi ameongeza kuwa, tawala za UAE, Bahrain na Saudi Arabia zimekuwa vibaraka wakubwa kiasi kwamba, zinaipatia fedha Marekani ili itekeleze mipango yao katika eneo hili.
Katibu Mkuu wa harakati ya Ansarullah ya Yemen amesema, watawala wa Saudi Arabia, UAE na Bahrain ni mamluki, wasaliti na tegemezi kwa maadui; na kushirikiana na tawala hizo ni usaliti na uhalifu na hakuna shaka kuwa tawala hizo zitashindwa.