Ismail Haniya, Mkuu wa Ofisi ya Kisiasa ya Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina (HAMAS) jana Jumanne alikutana na kufanya mazungumzo na Sayyid Hassan Nasrallah, Katibu Mkuu wa Harakati ya Hizbullah ya Lebanon mjini Beirut.
Kwa mujibu wa televisheni ya al-Manar ya Lebanon, viongozi hao wamejadili matukio ya hivi karibuni katika eneo la Asia Magharibi, na harakati za kambi ya muqawama dhidi ya adui Mzayuni.
Ofisi ya Habari ya Hizbullah imesema wawili hao wamejadili kwa kina Operesheni ya Upanga wa Quds na taathira zake kwa Wapalestina na kwa ulimwengu wa Kiarabu na Kiislamu.
Habari zaidi zinasema kuwa, Haniya na Sayyid Nasrallah wamesisitiza haja ya kuimarishwa uhusiano wa kidugu baina ya harakati za muqawama za Hamas na Hizbullah, pamoja na kugusia njia za kuhitimisha ukaliaji wa mabavu wa ardhi za Wapalestina unaofanywa na utawala ghasibu wa Israel.
Licha ya Wapalestina zaidi ya 250 wakiwemo wanawake na watoto wadogo kuuawa shahidi katika hujuma hiyo mpya ya utawala dhalimu wa Israel dhidi ya Wapalestina wa Gaza, lakini utawala huo wa Kizayuni hatimaye ulisalimu amri na kuomba vita hivyo visitishwe baada ya kupokea kipigo kikali kutoka kwa wanamuqawama.